Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar

Naibu Waziri wa Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makaazi Mhe. Juma Makungu Juma (wa pili kulia) akiwa katika eneo la Uwekezaji ambalo mhusika hajaliendeleza huko wilaya ya Kati Mkoa wa kusini Unguja

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imesema itawanyanganya umiliki wa ardhi wenyenji na wageni ambao walipewa kwaajili ya kuekeza lakini wameshindwa kuyaendeleza  hivyo sheria itachukua mkondo wake bila ya kumonea mtu muhali.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu waziri Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makaazi Zanzibar Juma Makungu Juma huko Wilaya ya kati Mkoa wa Kusini Unguja katika ziara maalumu ya kuyatembelea maeneo ambayo wageni na wenyeji walipewa kwaajili ya kuekeza lakini bado hawajaekeza.

Alifahamisha kwamba sheria ya Umiliki wa Ardhi, sheria Nam: 12 ya mwaka 1992 kifungu Nam 48 (1a) kinaeleza ukiukaji wa ukodishwaji ardhi (Violetion of the Restrictions in a lease) hivyo wizara yake itahakikisha inafata sheria kwa wawekezaji wakigeni na wazawa ambao walipewa maeneo kwa ajili ya uwekezaji na kutoyaendeleza kwa muda uliowekwa.

Alifahamisha kwamba lengo la ziara yake ni kuangalia pamoja na kuyatambua maeneo yote ya ardhi ambayo yametolewa na Serikali na kuwapa watu kwaajili ya kuekeza lakini bado wahusika wameshindwa kuyaendeleza kwa muda uliyowekwa.

Alisema Serikali  haina nia ya kumdhulumu mtu lakini kuna baadhi ya watu wameshindwa kuyaendeleza maeneo ambayo walipewa hivyo hakuna sababu ya kuwaachia umiliki wa ardhi mwekezaji huyo kwa sababu hakuna faida inayopatikana.

Aidha Naibu waziri Juma  ametoa wito kwa  wawekezaji wote walipewa maeneo ya ardhi kuhakikisha wanayaendeleza maeneo hayo kwani uwekezaji hutoa fursa nyingi za ajira kwa vijana pamoja na kuiongezea nchi mapato.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji Kamisheni ya Ardhi Khamis Juma Khamis amefahamisha kuwa  zoezi hilo linatarajiwa pia kufanyika katika maeneo yote ya uwekezaji ambapo hapo awali Kamisheni ya Ardhi ilishatoa taarifa kwa wawekezaji wote waliopatiwa lease ya ukodishwaji kuyaendeleza maeneo yao vyenginevyo sheria itachukua mkondo wake.

“Tulishawahi kutoa indhari kupitia vyombo vya habari kwa wawekezaji wote kuhakikisha wanayaendeleza maeneo yao lakini ziara ya leo tumebaini kuwa kuna maeneo bado yako vilevile nahayajaendelezwa chochote hivyo kwa sasa kinafuata ni utaratibu wa kisheri utatumika”Alisisitiza Khamis”

Nae Sheha wa Shehia ya Uroa Muhsini Amour Adam ametoa wito kwa wawekezaji ambao mpaka sasa bado hawajayaedeleza maeneo yao  kuitumia fursa hiyo kwa kuyaendeleza katika shughuli mbalimbali zikiwemo utalii kwa lengo la kukuza uchumi wa nchi.

Maeneo yaliyotembelewa na kuonekana kuwa bado hayajaendelezwa hadi sasa ni pamoja na pongwe,uroa na marumbi . Aidha kwa upande wa Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja ziara kama hiyo inatarajiwa kufanyika Mkoa wa Kaskazini Unguja.